CHAMA CHA MAPINDUZI
UMOJA NI USHINDI, AMANI NA MAENDELEO ...!!!

Sunday, September 26, 2010

Kikwete: Vyama vya upinzani ni 'fotokopi'



Jakaya Mrisho Kikwete
Ibrahim Bakari, Tarime na
Anthony Mayunga, Serengeti
MGOMBEA urais kwa tiketi ya kupitia CCM, Jakaya Kikwete jana alivinanga vyama vinavyoshindana kuwania kushika madaraka, akivifananisha na nakala za hati halisi (photocopy) na kuwataka wananchi kuviepuka.
Kikwete pia aliwatahadharisha wananchi wa mkoa huo, ambao hukumbwa na vita vya mara kwa mara vya koo, kuachana na chuki za kikabila akisema zinahatarisha amani ya nchi.

Akihutubia maelfu ya mashabiki na wapenzi wa CCM jana waliofurika kumsikiliza katika Uwanja wa Sabasaba mjini Tarime, Kikwete alisema chama chake kinastahili kupigiwa kura kwa vile kimedumisha amani na utulivu nchini.
"Msihangaike na vyama vya upizani ambavyo ni sawa na  'photo copy' wakati CCM ipo kuwaletea aendeleo," alisema Kikwete akirejea kauli yake aliyoitoa Agosti 20 wakati akizindua kampeni za CCM kwenye viwanja vya Jangwani jijini Dar es salaam.
Kuhusu vurugu zinazosababishwa na ukabila, Kikwete alisema suala hilo linachangia kuvunjika kwa amani miongoni mwa wana jamii.
"Angalieni kwa wenzenu hapo jirani, maana nyie mpo jirani zaidi mkivuka mpaka mnaingia kwa wenzenu. Wameumizana sana kutokana na ukabila," alisema akimaanisha nchi jirani ya Kenya ambayo ilikumbwa na mapigano mwaka 2007 baada ya kutangazwa kwa matokeo ya urais.

Alisema CCM ni chama kinachotekeleza sera zake, kudumisha amani na kuondoa udini na ukabila.
Hii ni mara ya kwanza kwa CCM kufanya mikutano yake mjini hapa ambako chama shindani cha Chadema kinashikilia jimbo hilo baada ya kushinda uchaguzi wa mwaka 2005 na uchaguzi mdogo wa mwaka 2008.
Shamrashamra zilianza majira ya saa 6:00 mchana kwa wakereketwa kukusanyika kwenye uwanja huo huku ikielezwa kuwa ni mara ya kwanza kwa chama hicho kukusanya watu wengi kiasi hicho.

Uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa wakazi wa maeneo jirani na uwanja huo walikodishiwa magari na CCM kuhakikisha kila mkereketwa wa chama hicho anahudhuria mkutano huo wa kampeni.
Mbali na hayo kikundi cha sanaa cha Tot Plus na wasanii wa kizazi kipya kwa pamoja walikuwa wakitoa burudani kwa pamoja kwa mashabiki hao wa CCM wanaokadiriwa kuwa zaidi ya 10,000.

Huku akishangiliwa na umati uliohudhuria mkutano huo, Kikwete alisema serikali itapambana kikamilifu na wezi wa mifugo na haitachoka, na zaidi wataliwezesha zaidi Jeshi la Polisi mkoani humo kupambana na wahalifu hao.
Alisema sekta ya elimu imeimarishwa kwa kuwa awali kulikuwa na shule 10, lakini sasa kuna shule 28 na kuongeza idadi ya wanafunzi wanaofaulu kutoka 4,925 hadi 18,250. JK aliahidi kuwa serikali itaboresha upatikanaji wa walimu bora zaidi, madarasa ya kisasa, maabara za kisasa na nyumba za walimu.
Kikwete, ambaye hotuba yake ilikuwa ikikatishwa mara kwa mara kwa kushangiliwa, aliwataka wakazi wa Tarime kujiepusha na ugonjwa hatari wa Ukimwi kutokana na takwimu zinazoonyesha kuna asilimia kubw aya maambukizi ya Ukimwi mkoani humo.
Kikwete alirejea kauli yake ambayo amekuwa akiitoa mara kwa mara kwa wanafunzi wanaopata mimba akiwaambia wakazi wa mkoa huo kuwa wanaoambukizwa Ukimwi wanaupata kwa ajili ya tamaa na viherehere vyao.

Alisema serikali yake pia inapambana na malaria kuhakikisha ugonjwa huo unatokomezwa.
Kuhusu huduma za maji, Kikwete alisema serikali ya CCM imejitahidi kuboresha sekta ya maji na tayari wamepata fedha kutoka Benki ya Dunia kwa ajili ya kuimarisha miradi ya maji na kwamba ndani ya miaka mitatu kila mkazi wa mkoa wa Mara atakuwa akitumia maji ya bomba.
Kikwete, ambaye pia ni mwenyekiti wa CCM, pia aliahidi kuboresha sekta ya kilimo kwa kuzalisha wataalam bora na kuweka ruzuku kwenye mazao kama kahawa.

Kikwete alitokea Shirati, Rorya na Serengeti ambako katika mikutano yake alisema chama chake kimeimarisha huduma za afya, kilimo na miundombinu kwa mkoa wa Mara na hata katika majimbo yanayoongozwa na wapinzani.
Akiwa wilayani Sengereti, Kikwete alikiri wazi kuwa ahadi ya CCM kujenga chuo cha ufundi stadi cha Veta wilayani humo haikutekelezwa, lakini akaahidi kuwa chama hicho kinajipanga kutekeleza ahadi hiyo katika kipindi cha miaka mitano ijayo.
Akihutubia mkutano wa kampeni kwenye Uwanja wa Mbuzi mjini Serengeti, Kikwete alisema kuwa waliyoahidi wametekeleza na ahadi nyingine zilizobaki watazitekeleza.

Mkutano huo ulipangwa kuanza saa 4, asubuhi, lakini hata hivyo ukafanyika saa 8.30 mchana huku ikidaiwa kuwa kuchelewa kuanza kulitokana na Kikwete kuendelea na mikutano ya kampeni wilayani Ngorongoro.

“Hapa sana sana ni Veta ambayo tuliahidi, lakini hatukuitekeleza. Sasa tutajenga katika miaka mitano ijayo, tutaweka umeme. Vijiji 13 vya jirani vitapata maji kwa kuwa Sh428 milioni zimetengwa kwa ajili hiyo. Kuhusu elimu tunategemea mwaka kesho (2011), kila mtoto awe na kitabu chake,” alisema Kikwete bila kufafanua sababu za kutojengwa kwa Veta.
Kuhusu ujenzi wa barabara ya lami ndani ya hifadhi ya Serengeti, mgombea huyo wa CCM alikiri kuwa siku moja baada ya kutangaza ujenzi wake Julai mwaka huu alipokuwa wilayani Serengeti, lakini siku iliyofuata dunia ilichamamaa kumpinga ikidai kuwa mpango huo unalenga kuua hifadhi ya Serengeti.

“Jamani wanamazingira walichachamaa sana, nasi tunazingatia hatutajenga barabara ya lami ndani ya hifadhi ya Serengeti, lakini tutajenga barabara ya lami nje ya hifadhi kwa wakazi wa Mugumu. Hiyo ni haki yake,” alisema.
Alisema tayari wameanza usanifu wa barabara hiyo na baada ya hapo watashughulikia tathimini ya kimazingira ili kuona madhara yake kwa ajili ya kuanza ujenzi.

Kuhusu uwanja wa ndege, Kikwete alisema utajengwa Serengeti ili wageni waweze kutua.
"Tuliahidi na tutajenga uwanja wa ndege ili wageni waweze kutua hapa,” alisema Kikwete bila kufafanua ujenzi huo utaanza lini.

Kikwete aliyeonyesha uchovu katika mkutano huo alishuka ghafla jukwaani na kuondoka baada ya kuwatambulisha wagombea ubunge, akiwaacha wananchi wakimsubiri.
Tukio lililotokea baada ya kupokea wanachama wapya 162 waliotajwa na katibu wa CCM wa mkoa, Ndegaso Ndekubali kuwa wametoka CUF, Chadema na NCCR-Mageuzi.

Mmoja wa waliojiunga na CCM jana ni Godfrey Paul aliyetambulishwa kuwa ni katibu wa Chadema wa Kata ya Magange aliyesema amerudi kwa baba na mama yake.

Hata hivyo, kuteremka ghafla jukwaani kwa Kikwete kulimaliza mkutano huo bila kufungwa rasmi huku wananchi wakibaki na maswali juu ya mustakabali wa mkutano huo uliofunguliwa na mwenyekiti wa CCM wilaya.
Marwa Mwita, mkazi wa Mugumu, alisema bado anajiuliza ilikuwaje mgombea huyo akaondoka bila ya kuaga.
"Hilo ni jambo la kujiuliza, lakini huenda amechoka na anasahau alitakiwa kufanya nini. Kwanza amechelewa kufika, hakuomba radhi, kahutubia mambo yale yale ya kila mwaka.

Julai mwaka huu wakati mgombea huyo alipozindua Bwawa la Manchira alizungumzia ujenzi wa barabara ya Serengeti na uwanja wa ndege, ahadi alizozirudia jana.

No comments: