CHAMA CHA MAPINDUZI
UMOJA NI USHINDI, AMANI NA MAENDELEO ...!!!

Sunday, October 27, 2013

UONGOZI WA TAWI LA CMM MOSCOW WAMUUNGA MKONO MWENYEKITI WA CHAMA TAIFA DR. JAKAYA MRISHO KIKWETE.

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete(katikati) akionyesha kuwa mwenye furaha, alipowasili ukumbini kufunga mafunzo kwa watendaji na viongozi wa CCM ngazi za wilaya na mikoa, juzi, 24-10-2013 mjini Dodoma. Mafunzo hayo yaliyokuwa ya siku nne yalifunguliwa na Makamu Mwenyekiti wa CCM, Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein. Kushoto ni Makamu Mwenyekiti wa CCM (Bara) Mhe.Philip Mangula na kulia ni Katibu Mkuu wa CCM, Mhe.Abdulrahman Kinana.


Mwenyekiti wa tawi la CCM Moscow Dr. Alfred Kamuzola pamoja na uongozi wote wa tawi kwa pamoja wameunga mkono kauli ya mwenyekiti wa CCM taifa Dr. Jakaya Kikwete aliyoitoa juzi wakati akifunga mafunzo kwa watendani na viongozi wa wilaya na mikoa wa Chama Cha Mapinduzi nchi nzima yaliyomalizika huko Dodoma juzi tarehe 24 oktoba 2013.

Mwenyekiti wa chama taifa Dr. Jakaya Kikwete ameonesha wasiwasi wake juu ya mafanikio ya chama katika uchaguzi wa serikali za mitaa mwakani (2014) na katika uchaguzi mkuu ujao ( mwaka 2015) kutokana na vitendo vya baadhi ya viongozi wa chama kutokuwa na maadili mema . Katika hotuba yake, Dr.Kikwete alisema, nukuu: Kama hatutabadilika katika suala la rushwa, mwaka 2015 tutakuwa na wakati mgumu sana, na kama mwaka huo tutafanikiwa kuishika serikali, basi mwaka 2020 hatutarudi tena madarakani…”.

“… Najua rushwa ipo na mnaendelea kupokea sh laki mbili za ‘airtime’ (muda wa mawasiliano), ndugu zangu hatutafika, ama wengine watavuka na wengine kukwama,” alisema. Mwisho wa kunukuu.

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akiwa na Katibu
Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana na Makamu Mwenyekiti
wa CCM (Bara) Philip Mangula, baada ya kuwasilini ukumbini
na kulakiwa kwa shangwe na wahitimu wa mafunzo kwa wa
watendaji na viongozi wa CCM ngazi za mikoa na wilaya nchini
mjini Dodoma.
Tawi linaunga mkono kauli hiyo kutokana na hali halisi kwamba katika chaguzi zijazo, chama kitakuwa na wakati mgumu sana ili kushinda. Ni lazima viongozi wabadilike kwa manufaa ya wanachama wao na watanzania wote. Mwenyekiti wa chama taifa kaonesha kusikitishwa na hali ilipofikia ya baadhi ya viongozi kufikia hatua ya kupokea rushwa kwa njia ya simu. Viongozi wa aina hiyo ni lazima waachie ngazi na wawajibishwe.

Hata katika utendaji, viongozi wa vyama vya upinzani kwa sasa wanafanya kila wawezavyo kukaa karibu na wananchi na kusikiliza shida kero zao mara kwa mara. Wakati viongoziw walio wengi kwa upande wa chama chetu hawafanyi vitu kama hivyo kwa kasi ambayo ingewavunja nguvu wapinzani. Lazima tujue kuwa kila nafasi inayopatikana, wapinzani wanaitumia kwa nguvu zote ili kujiimarisha hasa kwaajili ya chaguzi zijazo.

Kiongozi anapoonekana si muadilifu, basi ni lazima kuachia ngazi na chama kumwajibisha kwa manufaa ya chama na kwa kufanya hivyo tutaweza kujenga imani ya wanachama wetu. Kazi ya kujenga imani kwa wanachama ambao wamechoshwa na matendo maovu ya baadhi ya viongozi ndani ya chama ni kazi ngumu sana. Kwani ukishapoteza imani ya wanachama juhudi za kurejesha imani yao kwa chama tena zinagharimu muda na rasilimali maradufu ili angalau kuweza kurudisha imani ya wachache kati ya wengi ambao watakuwa wamepoteza imani kwa chama. 

Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete akizungumza wakati wa kufunga
mafunzo ya watendaji na viongozi wa CCM ngazi za 
wilaya na mikoa
hapa nchini, mjini Dodoma.
Ni viongozi mahiri na waadilifu tu ndiyo wanaweza kujenga tena imani ya wanachama kwa chama. Hivyo basi viongozi wala rushwa wasiendelee kukichafua na kukiua chama ambacho bado kina mapenzi mema kwa wanachama na kwa wananchi wote. Lazima tukilinde chama chetu kwa hali na mali dhidi ya viongozi na wanachama wasio waadilifu na wasio na nia nzuri ya kukijenga chama.

KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI.

No comments: